1. |
Alikunja kipaji na akageuka, |
2. |
Kwa sababu alimjia kipofu! |
3. |
Na nini kitakujuulisha pengine yeye atatakasika? |
4. |
Au atawaidhika, na mawaidha yamfae? |
5. |
Ama ajionaye hana haja, |
6. |
Wewe ndio unamshughulikia? |
7. |
Na si juu yako kama hakutakasika. |
8. |
Ama anaye kujia kwa juhudi, |
9. |
Naye anaogopa, |
10. |
Ndio wewe unampuuza? |
11. |
Sivyo hivyo! Huku ni kukumbushana. |
12. |
Basi anaye penda akumbuke. |
13. |
Yamo katika kurasa zilizo hishimiwa, |
14. |
Zilizo inuliwa, zilizo takaswa. |
15. |
Zimo mikononi mwa Malaika waandishi, |
16. |
Watukufu, wema. |
17. |
Ameangamia mwanaadamu! Nini kinacho mkufurisha? |
18. |
Kwa kitu gani amemuumba? |
19. |
Kwa tone la manii, akamuumba na akamkadiria. |
20. |
Kisha akamsahilishia njia. |
21. |
Kisha akamfisha, akamtia kaburini. |
22. |
Kisha apendapo atamfufua. |
23. |
La! Hajamaliza aliyo muamuru. |
24. |
Hebu mtu na atazame chakula chake. |
25. |
Hakika Sisi tumemimina maji kwa nguvu, |
26. |
Tena tukaipasua pasua ardhi kwa nguvu, |
27. |
Kisha tukaotesha humo nafaka, |
28. |
Na zabibu, na mimea ya majani, |
29. |
Na mizaituni, na mitende, |
30. |
Na bustani zenye miti iliyo songana baraabara, |
31. |
Na matunda, na malisho ya wanyama; |
32. |
Kwa manufaa yenu na mifugo yenu. |
33. |
Basi utakapo kuja ukelele, |
34. |
Siku ambayo mtu atamkimbia nduguye, |
35. |
Na mamaye na babaye, |
36. |
Na mkewe na wanawe – |
37. |
Kila mtu miongoni mwao siku hiyo atakuwa na lake la kumtosha. |
38. |
Siku hiyo ziko nyuso zitazo nawiri, |
39. |
Zitacheka, zitachangamka; |
40. |
Na nyuso siku hiyo zitakuwa na mavumbi, |
41. |
Giza totoro litazifunika, |
42. |
Hao ndio makafiri watenda maovu. |